Maisha, Huduma na Urithi wa Derek Prince.

Derek Prince alikuwa mwalimu wa Biblia wa kimataifa ambaye aliheshimiwa sana kwa ufahamu wake wa kitheolojia na imani ya Kikristo ya kweli. Yeye ni mwandishi wa vitabu zaidi ya 100 ambavyo vinaendelea kuvutia maelfu ya wasomaji wapya kila mwaka.

Derek Prince

Huduma
Mwalimu wa Biblia wa kimataifa, mwandishi, mchungaji, mmishonari na mwanatheolojia
Kuzaliwa:
Agosti 14 1915, Bangalore, India
Kufariki:
Septemba 24 2003 (akiwa na umri wa miaka 88), Yerusalemu, Israeli

Yaliyomo

(Bofya ili kusogeza hadi eneo)

Maisha ya awali

Derek Prince alizaliwa katika familia ya kijeshi kutoka Uingereza huko Bangalore, India mwaka wa 1915. Akiwa na umri wa miaka 14 alipata ufadhili wa masomo katika Chuo cha Eton ambako alisoma Kigiriki na Kilatini. Aliendelea na masomo yake katika Chuo Kikuu cha Cambridge, Uingereza, ambapo alipata mafunzo katika Falsafa ya Kale na ya Kisasa katika Chuo cha King. Zaidi ya hayo, Derek alisoma lugha kadhaa za kisasa alipokuwa akihudhuria Chuo Kikuu cha Cambridge, zikiwemo Kiebrania na Kiaramu, ambapo baadaye aliziboresha katika Chuo Kikuu cha Kiebrania huko Yerusalemu.

Ingawa Derek alilelewa katika Kanisa la Kianglikana, aliacha mizizi yake ya Kikristo akiwa katika Chuo Kikuu cha Cambridge na kushikilia mtazamo wa ulimwengu wa kutoamini kuwa kuna Mungu. Akitafakari kuhusu miaka hiyo ya masomo ya juu, baadaye alisema:

"Nilijua maneno mengi marefu na misemo, na nilikuwa nimejaribu vitu vingi tofauti. Lakini, nikitazama nyuma, ningelazimika kukiri kwamba nilikuwa nimechanganyikiwa na kufadhaika, nilivunjika moyo na kukata tamaa, na sikujua ni wapi ningepata jibu.”

Vita vya Pili vya Dunia

Kazi ya kitaaluma ya Derek ilitatizwa wakati Vita vya pili vya Dunia vilipoanza. Mnamo mwaka wa 1940 alijiandikisha katika Jeshi la Kifalme la Medical Corps kama askari asiyepigana kutokana na misingi ya imani yake binafsi. Ili kuendeleza masomo yake wakati wa utumishi wa kijeshi, Derek alibeba Biblia ambayo aliiona wakati huo kuwa maandishi ya falsafa badala ya Neno la Mungu lililovuviwa

Mnamo tarehe 31 Julai 1941, akiwa kwenye kambi ya mafunzo huko Scarborough, Yorkshire, alikutana na Yesu kwa nguvu ambayo ilibadilisha mkondo wa maisha yake. Akikumbuka tukio hili alisema:

“Nilisikia sauti ya Yesu, ikizungumza kwa uwazi sana kupitia maandiko, yaani Biblia. Na tangu siku niliposikia sauti yake, hadi leo, kuna mambo mawili ambayo sijawahi kutilia shaka. Sijawahi kuwa na shaka kwamba Yesu yuko hai, na sijawahi kutilia shaka kwamba Biblia ni Neno la Mungu.”

Ndivyo safari ya kiroho ya mmoja wa walimu wa Biblia mashuhuri zaidi wa karne ya 20 ilivyoanza.

Mara tu baada ya kumpokea Kristo, Derek alihamishwa kwenda kazini katika majangwa ya Afrika Kaskazini ambako alikaa miaka mitatu akihudumu kama daktari wa jeshi. Alitumia muda wake wa ziada kujifunza Biblia na kuimarisha uhusiano wake wa kibinafsi na Mungu.

Mwishoni mwa vita, Derek aliachiliwa kutoka kwa jeshi akiwa Yerusalemu,huku akishuhudia utimizo wa unabii wa Biblia kwa watu wa Kiyahudi kurudi kule Israeli.

Lydia Prince

Mnamo mwaka wa 1946, Derek alimuoa mke wake wa kwanza, Lydia Christensen, mmishonari kutoka Denmark ambaye alisimamia makao ya watoto karibu na Yerusalemu. Kwa kufanya hivyo, akawa baba wa wasichana wanane wa kuasili.

Derek na Lydia waliishi Yerusalemu hadi baada ya kuanzishwa kwa taifa la Kiyahudi la Israeli mnamo mwaka wa 1948. Walipojikuta kati ya vikosi vya Waarabu na Israeli wakati wa Vita vya Uhuru, walihamishwa kutoka nyumbani kwao na kwa kusita wakahamia Uingereza. Mara baada ya kuishi katikati mwa London, Derek alianza kuhubiri kwenye Speaker's Corner katika Hyde Park, mara nyingi akiandamana na Lydia na baadhi ya wasichana. Baada ya muda, waliohudhuria walialikwa nyumbani kwa huduma zaidi, na kanisa jipya likazaliwa. Hii iliendelea hadi mwaka wa1956 wakati familia ya Prince iliitikia wito wa Mungu na kuhamia Kenya kama wamishonari mnamo Januari mwaka wa 1957.

Katika miaka iliyofuata, Derek na Lydia waliona matunda mengi walipokuwa wakiwahudumia wenyeji, ikiwemo msichana mmoja ambaye alifufuliwa kutoka kwa wafu kupitia maombi.

Kufikia mwaka wa 1962, wenzi hao walikuwa wameasili mtoto mchanga Mkenya ambaye alikuwa yatima na walikuwa kwenye likizo nchini Kanada. Lydia, aliyemzidi Derek umri kwa miaka 25, alikuwa na umri wa miaka sabini na alitamani kukaa karibu na marafiki na waamini wengine. Akichochewa na hitaji hilo, Derek alikubali mwaliko wa kuwa mwalimu wa Biblia katika kanisa la Kipentekoste huko Minneapolis.

Derek na Lydia Prince.

Kabla ya mwisho wa muongo, hata hivyo,Familia ya Prince ilihama mara tatu zaidi; Seattle, Chicago na Fort Lauderdale, mtawalia. Maendeleo katika huduma yalifungua milango mipya isiyotarajiwa, lakini wenzi hao walibaki kuwa waaminifu kwa wito wa Mungu uliokuwepo kila wakati.

Kufikia mwaka wa 1968, huduma ya kufundisha ya Derek ilikuwa imekua kwa kasi katika vuguvugu lililoibuka la Karismatiki. Alisafiri sana, akihubiri Neno kwa nguvu na mamlaka.

Mnamo Oktoba 5, mwaka wa 1975, Lydia Prince alifariki akiwa na umri wa miaka 85 akiwa amezungukwa na familia yake. Yeye ndiye mwandishi wa kitabu cha "Kuteuliwa huko Yerusalemu""Appointment in Jerusalem" ambacho kilichapishwa muda mfupi kabla ya kifo chake mwaka huo huo.

Ruth Prince

Mnamo mwaka wa 1978, Derek alimuoa mke wake wa pili, Ruth Baker, mama Mmarekani aliyekuwa na watoto watatu wa kuasili. Walikutana Yerusalemu wakati Derek alipokuwa akizuru Israeli akiwa pamoja na marafiki.

Kwa pamoja, awamu mpya ya huduma iliibuka na uzinduzi wa kipindi cha redio cha kila siku kiitwacho "Leo na Derek Prince". Hapo awali kilitangazwa kwenye vituo nane vya redio, hadhira ilikua kwa haraka na urithi wa huduma ukaimarika. Leo, rekodi hizo zimesambazwa ulimwenguni pote na zinapatikana katika lugha mbalimbali.

Maelezo ya hadithi ya upendo ya Derek na Ruth yameandikwa katika kitabu "God is a Matchmaker" ambacho waliandika pamoja na kuchapishwa mnamo mwaka wa 1986.

Derek na Ruth Prince wapiga picha kando ya Mto Zambezi, Zambia, mwaka wa 1985.

Ruth aliaga dunia huko Yerusalemu tarehe 29 Desemba mwaka wa 1998 kufuatia ugonjwa wa muda mfupi ambao haukutambuliwa ipasavyo. Alikuwa na umri wa miaka 68 na alikuwa amehudumu kwa uaminifu kando ya Derek kwa zaidi ya miongo miwili.

Kutokana na huzuni, kisima cha uchungu kilianza kutanda moyoni mwa Derek. Akihisi kwamba kuna nguvu chafu ambazo mwishoye zingemtenga na Mungu, alitoa tangazo la hadharani kwenye mazishi ya Ruthu ambalo lilifafanua miaka yake iliyobaki. Jeneza lilipokuwa likishushwa, Derek alimshukuru Mungu kwa yote Aliyoyafanya katika maisha ya Ruthu, akithibitisha kwa kweli upendo na tumaini lake kwa Baba yake wa mbinguni. Akitafakari juu ya hatua hiyo, baadaye alisema:

"Ulikuwa wakati muhimu katika maisha yangu. Nilijua kamwe singeweza kuendelea na maombolezo niliyokuwa nayo juu ya Ruthu. Ningemlaumu Mungu kila wakati, na mlango wa maisha yangu ungefungwa. Hii ndiyo njia ya pekee ningeweza kuendelea.”

Kifo

Derek Prince alifariki kwa sababu za kawaida mnamo tarehe 24 Septemba 2003, akiwa na umri wa miaka 88. Alikuwa ameteseka kutokana na kudhoofika kwa afya yake kwa muda mrefu na aliaga akiwa usingizini mwake nyumbani kwake huko Yerusalemu.

Alizikwa kwenye Makaburi ya Kimataifa ya Alliance Church huko Yerusalemu, kaburi la Derek limeandikwa hivi:

DEREK PRINCE
1915 - 2003
AMEKWENDA NYUMBANI
Mwalimu wa Maandiko
Katika Ukweli na Imani na Upendo
Ambao upo ndani ya Kristo Yesu kwa ajili ya Wengi
Mungu ni Mwaminifu

Derek Prince akihubiri katika Kanisa la Trinity ( Kanisa la Cornerstone la sasa) huko San Antonio, Texas, mwaka wa 1974.

Mwalimu wa Biblia.

Mnamo mwaka wa 1944, akiwa kwenye bohari ya vifaa vya matibabu huko Kiriat Motzkin, Israeli, Bwana alizungumza na Derek kwa uwazi akisema:

"Umeitwa kuwa mwalimu wa Maandiko katika kweli na imani na upendo ulio katika Kristo Yesu - kwa ajili ya wengi."

Ilionekana kuwa mbali na kituo cha wakati huo cha Derek, lakini baada ya muda ilifanyika kama vile Mungu alivyoahidi katika mwaka wa 1941:

“Itakuwa kama kijito kidogo. Kijito hicho kitakuwa mto. Mto huo utakuwa mto mkubwa. Mto mkubwa utakuwa bahari.Bahari itakuwa bahari kuu, nayo itakuwa katikati yako; Lakini jinsi gani, lazima usijue, huwezi kujua, hutajua."

Hadi siku ya leo, jina Derek Prince bado linajulikana kwa theolojia nzuri na mafundisho ya Neno la Mungu yaliyo wazi lakini yenye utaratibu. Imani yake thabiti na kujitolea kwake katika kujifunza maandiko kulimgeuza kuwa mmoja wa walimu wa Biblia walioheshimiwa na kupendwa sana wakati wake.

Derek ni mwandishi wa zaidi ya vitabu 100 na hazina ya thamani kubwa ya nyenzo za mafundisho ya Biblia ambazo hudumisha kazi na shauku yake ya maisha. Zikitafsiriwa katika lugha zaidi ya 100, zinasalia kuwa chanzo cha msukumo na masomo kwa mamilioni ya Wakristo kote ulimwenguni.

Mwaka mmoja kabla ya kifo cha Derek mnamo mwaka wa 2003, mwandishi wa habari wa The Jerusalem Post alimuuliza ni hitaji gani kuu la Kanisa leo. “Walimu wa Biblia,” Derek akajibu, “walimu wa Biblia walio makini. Akikumbuka mazungumzo hayo, mwandishi wa habari aliandika mnamo mwaka wa 2006, "Kwa kweli, kumekuwa na wachache kama yeye."

Huduma ya Derek Prince

Mnamo Mei mwaka wa1971, Derek alifungua rasmi ofisi huko Fort Lauderdale, Florida, ili kuchapisha na kusambaza mafundisho yake. Hapo awali ilijulikana kama Derek Prince Publications, shughuli zilipanuka hatua kwa hatua, na mnamo Desemba mwaka wa 1990 ilipewa jina la Derek Prince Ministries.

Leo,Huduma ya Derek Prince ina ofisi katika zaidi ya nchi 45 duniani kote, zikiwemo Australia, Kanada, Uchina, Ufaransa, Ujerumani, Uholanzi, New Zealand, Norway, Russia, Afrika Kusini, Uswizi, Uingereza na Marekani. Imesalia kuwa na nia thabiti ya kuwahudumia walio na njaa ya kiroho, na kwa kufanya hivyo, kushikilia maono ambayo Derek alieleza Julai mwaka wa 2002:

“Ni shauku yangu, na ninaamini nia ya Bwana, kwamba huduma hii iendeleze kazi, ambayo Mungu alianza kupitia kwangu zaidi ya miaka sitini iliyopita, hadi Yesu atakaporudi.”
Derek Prince